Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

October 27, 2017

Mvua Yasababisha Madhara Makubwa Jijini Dar.......Watu 6 Wahofiwa Kusombwa na Maji

SeeBait
Mvua  iliyonyesha usiku wa kuamkia jana, iligeuka kuwa balaa baada ya kusababisha madhara makubwa, ikiwa ni pamoja na watu sita kutojulikana walipo na zaidi ya nyumba kubomoka eneo la Mbezi.


Kama ilivyo kawaida jijini Dar es Salaam, mvua hiyo iliharibu miundombinu ya usafiri ya maeneo kadhaa, ikisababisha baadhi ya barabara kutopitika na Kampuni ya Mabasi Yaendayo Kasi (Udart) kulazimika kusimamisha shughuli zake.

Udart imesema jana kuwa ilisitisha huduma kutokana na eneo la Jangwani, ambako kuna ofisi zake, kujaa maji hivyo kuathiri shughuli zake.

“Tumesitisha huduma za mabasi yote kutokana na eneo la Jangwani kujaa maji,” alisema mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano cha Udart, Deus Bugaywa.

Barabara kadhaa zilikuwa hazipitiki magari na watembeao kwa mguu, huku mitaa kadhaa ya maeneo ya Jangwani ikiwa imefurika maji na kusababisha wakazi kukimbilia Barabara ya Kigogo-Mabibo kushuhudia maji hayo, ambayo pia yalifurika hadi juu ya daraja la Kigogo Mwisho.

Wakazi wa maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam walikumbwa na mshangao jana alfajiri wakati walipokuta maeneo yao yamefurika maji kutokana na mvua hiyo iliyonyesha kuanzia juzi jioni na kuendelea usiku kuamika jana. Baadhi walishuhudia nyumba zao zikibomka na madaraja kukatika.

Mvua hizo zilisababisha daraja eneo la Mbezi kuvunjika na hivyo basi la daladala lililokuwa limebeba abiria kutoka Segerea kuelekea Mbezi Mwisho lilikwama daraja baada ya kuzidiwa na kasi ya maji yaliyofunika daraja hilo.

Abiria waliokuwa ndani ya daladala hilo waliokolewa wote huku mmoja wao akizimia na kupelekwa hospitali.

Mvua hiyo pia ilisimamisha shughuli za kijamii, wananchi walishindwa kwenda kazini wakiwamo wanafunzi ambapo walishindwa kufika shuleni kutokana.

Maji yalijaa barabarani huku shughuli za usafiri zikisimama , maduka na vibanda vya biashara vilifungwa na vingine vikisombwa na maji.

Pia mwenyeki wa Mtaa wa Kiluvya kwa Komba, Julius Mgini alisema watu sita wanasadikiwa kusombwa na maji eneo hilo akiwamo mtoto mmoja na nyumba za familia tatu zimebomoka.

“Katika eneo langu kuna daraja limekatika na watu sita wanasadikiwa kusombwa na maji. Waliosombwa ni pamoja na mtoto mdogo ambaye bado hatujajua umri wake,” alisema.

Hata hivyo, kamanda wa Polisi wa Kinondoni, Jumanne Muliro alisema bado wanakusanya taarifa za mafuriko hayo na baadaye kuzipeleka kwa kamanda wa Kanda ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa.

Kamanda Mambosasa pia alisema wanafanya tathimini ili kujua athari za mafuriko.

==> Picha zote na Iman Nsamila


No comments: