Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

October 27, 2017

Kampuni ya Barrick Yatenga Dola Milioni 300 kuilipa Serikali ya Tanzani........Lakini kwa Masharti Haya!



SeeBait
Licha ya kupata hasara kwenye robo ya tatu ya mwaka, kampuni ya Barrick imetenga dola 300 milioni za Marekani (zaidi ya Sh660 bilioni) kuilipa Serikali, lakini imeweka sharti; inataka iruhusiwe kusafirisha makinikia.

Acacia, kampuni tanzu ya Barrick na inayomiliki migodi ya Bulyanhulu na Buzwagi, imezuiwa tangu mwezi Machi kusafirisha mchanga huo wa madini kwenda kuuyeyusha nje ya nchi kwa ajili ya kupata mabaki ya dhahabu, shaba, fedha na madini mengine yaliyoshindikana kuchenjuliwa migodini.

Baada ya majadiliano baina ya Serikali na Barrick, kampuni hiyo ya Canada ilikubali kulipa dola 300 milioni “kuonyesha uaminifu”.

Taarifa ya miezi mitatu ya Barrick (Julai-Septemba) iliyotolewa juzi, inaonyesha kuwa ilipata hasara ya dola 11 milioni (zaidi ya Sh24 bilioni) tofauti na faida ya dola 175 milioni (zaidi ya Sh385 bilioni) iliyopata katika kipindi kama hicho mwaka jana (dola moja ya Kimarekani ni sawa na takriban Sh2,200 za Tanzania).

“Kupungua kwa mapato kunatokana na kushuka kwa uzalishaji na bei ya dhahabu pamoja na zuio la kusafirisha makinikia ambalo Serikali ya Tanzania iliiwekea Acacia,” inasema ripoti hiyo.

Vilevile, Barrick inasema kupungua kwa mapato yake kumechangiwa na ongezeko la makadirio ya kodi yanayofika dola 172 milioni (zaidi ya Sh378 bilioni) zilizopendekezwa kwenye majadiliano ya mustakabali wa operesheni za Acacia nchini.

Wakati Barrick ikitenga kiasi hicho cha kodi, Acacia ina dola 128 milioni (zaidi ya Sh282 bilioni) na kufanya jumla ya dola 300 milioni zilizokubaliwa kwenye mazungumzo yaliyofanyika kwa miezi mitatu iliyopita.

Masharti hayo si ya kwanza, itakumbukwa kwamba siku chache baada ya mkutano wa kukabidhi ripoti ya majadiliano hayo, kampuni ya Acacia ilisema haiwezi kulipa Dola 300 milioni kwa mkupuo na kwamba Barrick inajua hilo.

Ofisa fedha mkuu wa Acacia, Andrew Wray alinukuliwa na vyombo vya habari akisema: “Hatuna huo uwezo kuilipa Tanzania ili tumalizane kwenye mgogoro wa kodi uliopo.”

Wray alisema hayo Oktoba 20 wakati Acacia ilipokuwa ikiwasilisha ripoti yake ya fedha kwa robo ya tatu ya mwaka iliyoishia Septemba, ikionyesha kushuka kwa mapato na faida ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka jana.

Barrick imeiunga mkono Acacia kwenye msimamo wake kuhusu malipo hayo ya dola 300 milioni ikisema: “Kutokana na hali ya Acacia kifedha, malipo haya yanapaswa kufanywa kwa awamu yakitegemea mauzo ya dhahabu na usafirishaji wa makinikia.”

Katika robo hiyo ya tatu, faida ya Acacia imeshuka kwa asilimia 70 kutoka dola 52.878 milioni (zaidi ya Sh116.331 bilioni) mpaka dola 16.038 (zaidi ya Sh35.283 bilioni).

Wakati wa mkutano na vyombo vya habari uliofanyika Ikulu, Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi ambaye alikuwa mwenyekiti wa wawakilishi wa Serikali alisema Barrick wamekubali kutekeleza masharti yote ya sheria mpya ya madini.

Lakini kwenye taarifa yake, kampuni hiyo inasema itaendelea kuzungumza na Serikali ili kuondoa zuio la kusafirisha makinikia na kwamba mazungumzo hayo yataenda sambamba na kutafuta suluhu ya deni la kodi la kiasi cha dola 190 bilioni (zaidi ya Sh424 trilioni) ambazo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeitoza Acacia ikiwa ni malimbikizo ya kodi, faini na riba.

“Tunatarajia mazungumzo haya yatakamilika ndani ya nusu ya kwanza ya mwaka ujao,” inasema Barrick.

Pamoja na hasara hiyo ya robo ya tatu, kwa miezi yote tisa, Barrick imepata faida ya dola 1.752 bilioni (zaidi ya Sh3.854 trilioni) ambayo ni zaidi ya mara saba ikilinganishwa na iliyopata kwa muda kama huo mwaka jana. Mwaka uliopita, ilitangaza faida ya dola 230 milioni (zaidi ya Sh506 bilioni).

Mbali na taarifa hiyo ya fedha, Barrick imefafanua kwa wadau wake kuhusu makubaliano yaliyoafikiwa kwenye majadiliano ya miezi mitatu baina yake na Serikali.

Chanzo: Mwananchi

No comments: