Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

July 19, 2013

WACHIMBAJI MADINI WILAYANI LUDEWA WATAKIWA KULIPA USHURU



 Madiwani wa halmashauri ya wilaya Ludewa wakiwa katika kikao
Afisa maendeleo ya jamii wilaya ya Ludewa Bw.Wiliam Malima akijibu hoja

 Baadhi ya wakuu wa Idara mbalimbali wakifuatilia kikao cha baraza la madiwani




Baraza la Madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Ludewa mkoani Njombe limemtaka mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuwafuatilia wachimbaji wadogo na wakubwa wa madini wilayani huo ili waweze kulipia ushuru kwa kazi wanazozifanya.

Akizungumza katika kikao cha baraza hilo jana mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Ludewa Mh.Matei Kongo alisema kumekuwa na wachimbaji wengi wenye maeneo ya madini wilayani humo wakifanya kazi zao lakini hakuna wanachokilipa kwa Halmashauri.

Mh.Kongo alimtaka Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kuwafuatilia wote wenye vitalu vya madini wilayani humo bila kujali ni wachimbaji wakubwa au wadogo wa ndani ya nchi au wanje ya nchi ili waweze kulipia kodi katika halmashauri.

Alisema taarifa zinaonesha kwa mwaka 2012 ni kampuni moja tu ya M.M.I LTD ndiyo iliweza kulipa kiasi cha shilingi laki nne lakini kumekuwa na wamiliki zaidi ya 54 wa vitaru vya madini wasiotambua uwepo wa ofisi za halmashauri kwaajili ya kulipia ushuru huo.

Tunashangazwa na kitendo cha wamiliki hawa wa vitaru kutolipa ushuru katika wilaya yetu wakati wanatumia barabara zetu huko vijijini na zinapokuwa mbovu ni Halmashauri pekee ndiyo inayowajibika kuzikarabati,hivyo tunakuagiza mkurugenzi kuwafuatilia wachimbaji hawa na kuwadai ushuru mara moja”,alisema Mh.Kongo.

Aidha mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Bw.Wiliam Waziri aliahidi kuwafuatilia wawekezaji hao katika ofisi zao ili kuweza kuzungumza nao namna ya ulipaji ushuru huo ambapo kwa miaka mingi wamekuwa wakwepa kuilipa Halmashauri hiyo.

Bw.Waziri alisema ofisi yake ilikuwa katika mchakato huo na kufuatia maagizo hayo ya Baraza la madiwani basi wamiliki wa vitaru hivyo watafuatiliwa na kuweza kupata maelezo ni kwanini hukwepa kulipa ushuru kutokana na kazi wanazozifanya wilayani hapo.

MKUU wa wilaya ya Ludewa Bw.Juma Solomon Madaha aliwataka madiwani wa Halmashauri ya wilaya ya Ludewa kushirikiana kikamilifu na watendaji wa halmashauri hiyo ili kuhakikisha ushuru huo unaisaidia halmashauri katika kukamilisha miradi ya maendeleo 
 
Alisema kuwa hakuna haja ya madiwani kusubiri vikao vya baraza ili kuwakosoa watendaji na badala yake ni kutoa ushirikiano kwa watendaji hao ili kuhakikisha miradi ya maendeleo inakamilika kwa wakati uliopangwa ili kuifanya wilaya hiyo kuwa na maendeleo haraka.

Bw.Madaha alisema njia sahihi ya kuisaidia halmashauri hiyo kujiendesha ni lazima kubuni vyanzo vya mapato ya ndani na si vinginevyo kwani kwa kubuni njia za kuongeza mapato ya halmashauri kunaweza kusaidia kutatua matatizo madogomadogo yanayojitokeza.

kimsingi kuna vyanzo vingi vya mapato wilayani hapa lakini hatuvitendei kazi kama vyanzo hivyo vitafuatiliwa hasa wawekezaji wa migodi wakubwa na wachimbaji wadogo wanapaswa kulipa ushuru katika Halmashauri yetu kwa kazi wanazozifanya”,alisema Bw.Madaha.

Alisema kutokana na shughuri za uchimbaji zinazofanywa na wachimbaji wadogo na makampuni makubwa ni dhahiri wanatakiwa kuilipa halmashauri kodi kwani wanatumia barabara zinazojengwa na Halmashauri hivyo si vyema kukwepa kulipa ushuru.

Bw.Madaha aliwataka madiwani na watendaji kushirikiana kimakilifu kwani hata yeye atakuwa mstari wa mbele ili kuhakikisha Halmashauri inainuka kimapato zaidi tofauti na wilaya nyingine.

Mwisho.

No comments: