Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

July 11, 2014

WATOTO WANAOISHI KATIKA MAZINGIRA HATARISHI WILAYANI LUDEWA WAANDALIWA MPANGO MKAKATI .




 Mratibu wa shirika la MLADEA Bw.Emmanuel Kayombo akisoma taarifa ya mradi kwa washirki
 washiriki wa warsha wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya kuanza mafunzo
 Wawezeshaji wakijadiliana jambo kabla ya kuanza mafunzo
             washiriki wakimsikiliza wezeshaji

Shirika la Mlangali Development Association(MLADEA) lenye makao yake makuu katika kata ya Mlangali wilayani Ludewa katika mkoa wa Njombe kwa kushirikiana na Halmashauri ya wilaya ya Ludewa kupitia ufadhiri wa The foundation for civil society wameandaa mpango mkakati utakaoweza kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wilayani hapa.

Akisoma taarifa ya maandalizi ya mpango mkakati huo mratibu wa shirika la MLADEA Bw.Emmanuel Kayombo alisema mradi huo wa kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi utatekelezwa katika tarafa ya mawengi wilayani hapa kutokana na takwimu ya watoto hao kuwa juu tofauti na tarafa nyingine.

Bw.Kayombo alisema wilaya ya Ludewa ambayo ilianzishwa rasmi Novemba 28 mwaka 1975 na kuwa Halmashauri ya wilaya Julai 1mwaka 1984 kwa sheria namba 5 ya Serikali za mitaa,sura ya 287 na kufanyiwa marekebisho yake mwaka 2002 ina jumla ya tarafa 5 kata 25,vijiji 77 na vitongoji 340 ina jumla ya watu 133281.

Alisema kulingana na taarifa ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 inaonesha kuwa tarafa ya Mawengi ina jumla ya watu 23768 ikiwa me 13721 na ke 10047 ambapo tarafa ina jumla ya kata 3 na vijiji 10 hivyo bado kumekuwa na uelewa mdogo kwa wananchi kuhusiana na sera na sheria mbalimbali ikiwemo sera na sheria ya haki za mtoto hali inayosababisha kushindwa kuthaminiwa.

“Asasi za kiraia kwa kushirikiana na halmashauri ya wilaya ya Ludewa tungependa kuwa na wananchi wenye maisha bora na endelevu ifikapo mwaka 2025 hivyo ni wajibu wa asasi zote kuandaa mipango mikakati kwa kushirikiana na wafadhiri ili kutoa elimu kwa wananchi katika kuandaa kamati za watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi kwa kila kijiji na mitaa ambazo zitawasaidia watoto hawa ambao wametelekezwa”,alisema Bw.Kayombo.

Bw.Kayombo alisema jamii ya tarafa ya Mawengi imekuwa haiwathamini watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi kutokana na ukosefu wa elimu hali ambayo itasababisha kuwa na waharifu wengi kutokana na kutothaminiwa na jamii inayowazunguka.

Aisha mwezeshaji wa mpango huo ambaye ni ofisa maendeleo ya jamii katika halmashauri ya wilaya ya Ludewa Bw.Thomas Kiowi alisema ifike wakati jamii inapaswa kutambua watoto hao ni miongoni mwa wanajamii kwani wakithaminiwa na kuendelezwa wanaweza kuwa viongozi wazuri kutokana na hali halisi ya maisha yao wanavyoishi.

Bw.Kiowi alisema imekuwa kawaida katika jamii kuona watoto hao ni mali ya Asasi za kiraia na wafadhiri hali ambayo si kweli hivyo kupitia kamati za watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi watoto hao ni mali ya jamii na jamii inapaswa kuwasaidia watoto hao katika michango mabalimbali ikiwemo ya mavazi na chakula kama wanavyoishi watoto wengine.

Alisema kuna baadhi ya maeneo tayari jamii imehamasika kutokana na kupata elimu hivyo tayari kila familia au kaya imekuwa ikitenga chakula na bajeti nyingine kwaajili ya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi kwa kupitia kamati zilizochaguliwa na wanajamii wenyewe hali ambayo inatia moyo na watoto hao wanaishi maisha ya kawaida kutokana na kuthaminiwa.

Bw.Kiowi aliwataka wanajamii wa tarafa ya Mawengi kwa kushirikiana na shirika la Mladea kuunda kamati hizo haraka ambazo zitasimamia na kutoa elimu kwa wananchi namna ya kuwasaidia watoto hao hata kama wafadhiri watasitisha misaada yao lakini jamii itakuwa na uwezo wa kuwaendeleza kielimu na huduma nyingine.

No comments: