Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

November 13, 2013

DC LUDEWA AZITAKA ASASI ZA DINI KUWEKEZA WILAYANI LUDEWA




MKUU wa wilaya ya Ludewa Bw.Juma Solomon Madaha amezitaka asasi za kidini kuwekeza katika maeneo mbalimbali wilayani Ludewa ili kuweza kujiongezea uwezo wa kujiendesha kwani bila kufanya hivyo asasi hizo zinaweza kuwa tegemezi kwa wafadhiri.

Bw.Madaha aliyasema hayo katika kanisa la Kirutheli wilayani Ludewa ambapo wajumbe mbalimbali wa kanisa hilo kutoka wilaya za mkoa wa Njombe wanahudhuria mkutano wa siku tatu wa kiroho ambao umeandaliwa na uongozi wa jimbo la mkoa huo.

Alisema kuokana na hali halisi ya wilaya ya Ludewa kwa sasa ambapo Mei 2014 ujenzi wa viwanda vya chuma katika mgodi wa Liganga na ufuaji umeme katika majimbo ya Mchuchuma unatarajia kuanza asasi za kidini hazina budi kujipanga katika kuwekeza maeneo ya Ardhi ili kuweza kujitengemea zaidi katika kuhudumiaa jamii.

Bw.Madaha alilishukuru kanisa la kiinjili la Kilutheri na makanisa mengine kwa kuwa bege kwa bega katika kushirikiana na Serikali katika kuihudumia jamii hasa maeneo ya Elimu,Afya na ujenzi wa maadili miongoni mwa vijana ambao wamekuwa wakimomonyoa maadili kila siku.

“kutokana na ujio wa wawekezaji wilayani Ludewa tunatarajia kuwa na watu wengi ambao watafanya kazi katika miradi ya Liganga na Mchuchuma hivyo ninyi kama asasi za kidini ni vema mngeanza kuwekeza katika sekta mbalimbali ili kuacha utegemezi kwa wafadhiri,kwa kufanya hivyo mtaongeza ajira kwa waamini wenu na kuwa na maisha bora”,alisema Bw.Madaha.

Alisema wananchi wa wilaya ya Ludewa wameanza kuandaliwa katika kutumia fulsa zilizopo ili kunufaika na miradi hiyo mikubwa  hivyo hata asasi za kidini zote nchini zinakaribishwa kuwekeza wilayani Ludewa kwani kwa kuchelewa kwao kushika maeneo ya uwekezaji asasi zitashindwa kufaidika na fulasa za migodi,

Kuhusiana na suala la maambukizi ya gonjwa la ukimwi Mkuu huyo wa wilaya aliwataka viongozi wa dini kuhubiri zaidi maadili na utii wa amri za mwenyezi Mungu kwani mpaka sasa mkoa wa Njombe unaongoza kwa 14.5% ya ukimwi kwa Tanzania ikifuatiwa na mikoa mingine.

Bw.Madaha alisema kama waumini watahubiliwa kuacha dhami ya zinaa basi sifa hiyo mbaya ya mkoa wa Njombe kuongoza katika suala la maambukizi ya ukimwi litakwisha na ongezeko la watoto yatima na wa mtaani litapungua kwa kiasi kikubwa.

Alisema suala la maambukizi ya ukimwi linasababishwa na mmomonyoko wa maadili kuanzia ngazi ya familia hivyo kuongoza katika suala hilo sio sifa nzuri hivyo kila kiongozi wa Dini aliyoko mkoa wa Njombe anapaswa kulitilia mkazo suala hilo ili kutoka katika sifa hiyo mbaya nchini.

No comments: