Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

September 29, 2013

MWALIMU MKUU KYELA ATUHUMIWA KWA UFISADI




MGOGORO mkubwa wa tuhuma za kifisadi zimeibuka Katika Shule ya Msingi Malungo iliyopo Kijiji Cha Kasala Kata ya Mwaya wilayani Kyela Mkoani Mbeya baada ya Serikali ya Kijiji hicho kumtuhumu Mkuu wa shule hiyo Benjamin Said kutumia vibaya Fedha za Ruzuku,madawati na michango mingine ya wananchi pamoja na matumizi mabaya ya madaraka.

Tuhuma hizo ziliibuliwa na mmoja wa wajumbe wa kamati ya shule Kijijini humo na kupelekea kufanyika kwa mkutano ambao haukufikiwa muhafaka na kupelekea Diwani wa Kata hiyo Aroub Kinana kumkamata Mwalimu huyo na kumpeleka kwenye kituo kikuu cha polisi Wilaya ambao walimuweka Lumande na baadaye alikuja kuwekewa dhamana na viongozi kutoka Ofisi ya Elimu Msingi.

Akizungumza leo na waandishi wa habari Kijijini humo Mwenyekiti wa Kijiji hicho Seti Mwakasekele alisema kuwa Mwalimu huyo ni tatizo katika Shule hiyo kwani amekuwa akiyatumia vibaya madaraka yake na kuwa wao wanamtuhumu kwa ufujaji wa fedha mbalimbali zitokazo Serikalini pamoja na michango ya wananchi bila kuwashirikisha wenzie.

Mwakasekele alizitaja tuhuma hizo kuwa ni Fedha za Madawati Tsh,720,000.Ruzuku kutoka Serikalini Tsh,1.888.000,michango ya watoto wa chekechea Tsh,30.000,Fedha za ukarabati wa shule Tsh,4,77,600,pamoja na michango mengine ya wananchi,na kuwa matumizi  ya fedha hizo Mwalimu huyo ameshindwa kuzitolea maelezo.

Kutokana na utata huo Halmashauri ya Kijiji iliamua kuitisha kikao cha dharula na kuwaita waalimu wote mbele ya mratibu elimu kata Diwani na Afisa mtendaji ambapo walimtaka mwalimu huyo atoe maelezo kuhusu utata wa fedha hizo na kuwa aliposhindwa kutoa maelezo waliamua kumpeleka polisi ambapo aliamua kuandika barua ya kukiri kuwepo na ufujaji huo na kuahidi kuzilipa fedha hizo tarehe 23.09.2013.

Aliongeza kuwa ilipofika siku hiyo hawakuona fedha yeyote aliyolipa zaidi ya kuletewa lisiti za kufoji ambapo uongozi wa Kijiji hicho hawakukubaliana na lisiti hizo na ndipo walipoitisha kikao cha pamojo siku ya tarehe 27.09.2013 kilichowashirikisha viongozi kutoka Idara ya elimu ikiongozwa na Afisa elimu taaluma Kassim Mtiro,kamati ya shule na wadau mbalimbali na katika majadiliano Idara ya elimu iliahidi kumleta mkaguzi ili kujua ukweli wa jambo hilo.

Afisa mtendaji wa Kijiji hicho Ambele Mwandobo alikiri kuwepo na tuhuma hizo na kuwa Halmashauri kupitia Idara ya elimu msingi wameahidi kumleta mkaguzi wa ndani siku ya juma tano ili afanye ukaguzi wa  kubaini tatizo hilo.

Afisa elimu msingi wa Wilaya ya Kyela Cloud Bulle kwa upande wake mbali na kukiri kuwepo kwa tukio hilo alidai kuwa wanakijiji ambao ndiyo wenye shule wanamtuhumu Mwalimu huyo na wao kama Idara watamtuma mkaguzi wa ndani wa Halmashauri ili afanye uchunguzi ili kubaini ukweli wa tatizo hilo na wao watachukua hatua stahiki pindi watakapo baini kuwepo na ufujaji huo.

Bulle aliongeza kuwa tatizo kama hilo liliwahi kutokea katika shule ya msingi Tenende kata hiyo hiyo ya mwaya ambapo walimtuma mkaguzi ambaye alibaini kuwepo kwa ufujaji na wao kama Idara ndani ya Halmashauri waliamua kumshusha cheo mwalimu huyo na kumuamuru alipe fedha zote alizoiba na tayari wanamkata mshahara hadi pale deni litakapomalizika.
Mwisho.
 Na Ibrahim Yassin,Kyela
0767269996.0653369996.


No comments: