Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

June 25, 2013

WANAWAKE WAPATA MAFUNZO KUHUSU HAKI YA KUMILIKI ARDHI. WASEMA MFUMO DUME SASA BASI.




WANAWAKE 70 kutoka katika vijiji saba vya kata za Lugarawa na Mundindi wilayani Ludewa katika mkoa wa Njombe wamepata mafunzo  ya uelewa juu ya haki  yao ya msingi ya kumiliki ardhi na kuondokana na mila potofu zinazotokana na mfumo dume nchini.

Mafunzo hayo ya kuwajengea uwezo yameandaliwa na shirika lisilokuwa la kiserikali la Ludende Development Assocition (LUDA) na kufadhiriwa na The Foundation Civil Society (FCS) la jijini Dar es Salaam ambapo Wanawake 70, Maafisa watendaji Kata, Maafisa Maendeleo ya jamii na Madiwani wa Kata hizo walihudhuria.

Akifungua mafunzo hayo Bw Labani Shagama ambaye ni Mratibu wa mradi wa haki ya mwanamke kumiliki ardhi alisema nia na madhumuni ya mradi huu ni kuhakikisha wanawake wanaelewa vyema haki zao za msingi ili waweze kuzilinda na kuzitetea wao wenyewe.

Bw Shagama alisema wanawake wengi wamekuwa wakiishi kwa hofu kutokana na kukandamizwa na  kutawaliwa na mfumo dume ambao kwa kiasi kikubwa umewaathiri hata kisaikolojia na kupelekea kunyanyaswa bila sababu ya msingi na wao kuishia kulalamika kimyakimya wasijue la kufanya.

“” Akaongeza kuwa serikali imeingia mkataba wa kuchimba madini ya makaa ya mawe ya mchuchuma na chuma cha Liganga je wanawake wanazijua haki zao za msingi watakazopata kutoka kwa mwekezaji moja kwa moja na serikali kwa upande mwingine ? “” Shagana aliwauliza wanawake hao

Washiriki hao wa Semina walionekana kutokujua lolote kuhusu wawekezaji hao wala taarifa ya nini kilichomo ndani ya mkataba ulioingiwa kati ya Serikali na wadau hao wa madini ingawa katika mikutano ya hadhara wanatangaziwa kuwepo kwa wawekezaji hao.

Bw Shagama aliwaambia washiriki hao kuwa kila mtu anayohaki ya kumiliki mali na mali hiyo yawezakuwa pesa au mali yoyote ikiwemo ardhi. Kadhalika sheria namba 5 ya ardhi ya mwaka 1999 na namba 2 ya mwaka 2002 zimeweka bayana juu ya umiliki wa ardhi sanjari na sera ya maendeleo ya mwanamke ya mwaka 2002, iko wazi juu ya wanawake kumiliki ardhi. 

Kwa nyakati tofauti Wanawake hao walilaumu serikali kutowapelekea elimu hiyo mapema na kwamba kama wangeipata mafunzo hayo wakiwa wasichana wasingekuwa wanakabiliwa na umaskini unaotokana na mila potofu zinazowapa wananume nguvu na nafasi ya kuwatumikisha wanawake kama wanyamakazi hukuwakiambulia ugali tu.

Kwa mujibu wa kifungu cha 4.2(b) mwanamke anayohaki ya kumiliki ardhi, kupata na kugawa ardhi sawa kwa masharti yaleyale kama ilivyohaki kwa mwanaume katika kifungu cha 3(2) cha sera. Ili kuhakikisha mikakati hiyo inatekelezwa sera imeeleza kuwa ugawaji na upatikanaji wa ardhi utakuwa sawa kwa raia wote.

Mariam Kiswaga pia alikuwa mmoja wa washiriki aliyeuliza swali kuwa baadhi ya wazazi hasa wazee watagawaje ardhi kwa watoto wao ambao walishaolewa na tayari pia wana watoto wao? 

Mwezeshaji Bwana Mligo alieleza kuwa kwa wale ambao tayari walishaolewa na wanafamilia zao mpango huu utakuwa ulishawapita ila wao sasa kama wazazi  wanalojukumu la kugawa ardhi bila kujali jinsia, hivyo watoto wote wagawiwe sawa

Mshiriki mmoja aliyejulikana kwa jina la Maria N. Mhagama alipopewa nafasi ya kushukuru kwa semina hiyo katika siku ya tatu ya semina aliomba kuwa shirika la LUDA liangalie namna ya kusambaza elimu hii kwenye kata za jirani wanazopakana “sisi sasa tumekombolewa kwani tutamiliki na kumilikisha ardhi” na ikiwezekana waende mbali zaidi ya kutoa elimu juu ya haki za wajane kwani pamoja na wanawake wakawaida kukabiliwa na tatizo la umiliki wa ardhi lakini pia ipo shida inayowapata wajane pindi waume zao wanapokufa.

Sheria ya ardhi ya kijiji namba 5 ya mwaka 1999,sheria namba 2 ya 2002 na sera ya mwaka 2002, sheria za kimila hazitatumika wala kupewa uzito kama zitambagua mwanamke, watoto na wenye ulemavu katika kupata, kumiliki ardhi ya kijiji. Ni lazima wahusika waeleze kuwa mwanamke anayohaki ya kushiriki katika maamuzi ya kijiji kwa maana kuwa kila mtu anayohaki ya kupata na kumiliki ardhi kwa ajili ya matumizi ya msingi.

Kata za Lugarawa na Mundindi ni Kata ambazo zimo ndani ya migodi ya chuma yaani Liganga na Maganga Matitu lakini wananchi wa maeneo hayo hawajui nini kinaendelea hadi sasa zaidi ya kushuhudia magari yakimiminika katika eneo hilo kila kukicha na wala hawajui haki zao migodi hiyo itakapoanza.


                                mwisho
Na Bazil Makungu,Ludewa.

No comments: