Social Icons

Facebook Twitter LinkedIn Google+

November 19, 2013

UHARIBIFU WA MAZINGIRA UNAOENDELEA WILAYANI LUDEWA NANI ALAUMIWE?.

 Mazingira yaliyoharibiwa kwa kuchomwa moto wilayani Ludewa



 Mkuu wa wilaya ya Ludewa Bw.Juma Solomon Madaha akilieleza baraza la Halmashauri namna ya kuyahifadhi mazingira



Uharibifu wa mazingira sio suala geni katika masikio ya jamii za Kiafrika lakini athari zake ni kubwa tofauti na matarajio ya uharibifu huo kwani kunabaadhi ya wananchi huharibu mazingira kwa makusudi bila kujua athari za baadae.

Jamii ya mkoa wa Njombe hasa katika wilaya ya Makete na Ludewa kumekuwa na uharibifu mkubwa wa mazingira kutokana na kilimo cha kuhama hama katika vijiji vya pambezoni mwa ziwa nyasa wilayani Ludewa na uandaaji wa msimu wa kilimo unaolazimu mashamba kuchomwa moto na kuunguza misitu ya asili.

Upitapo wilaya ya Ludewa na Makete sio kitu cha kushangaza uonapo safu za milima ya Living stone huonekana kuwa na rangi nyeusi hali hiyo huashiria moto umeshaunguza misitu yote ya asili na kuacha jivu nene juu ya milima hiyo msimu wa kiangazi.

Pia wakati mwingine milima hiyo ukiwa mbali huonekana kana kwamba inaukungu mzito lakini ukweli ni kwamba ukungu huo ni moshi mkubwa kutokana na uchomaji moto uliokithiri katika safu za milima hiyo ambayo ikitunzwa vizuri ni kivutio kwa watalii wanaokuja kutembelea misitu ya sasili na viumbe vinavyo patikana katika safu ya milima Livingstone.

Wilaya ya Ludewa ni moja ya wilaya Nchini yenye vivutio vingi vya utalii hasa misitu ya asili lakini ni wilaya ambayo kwa mwaka 2013 mazingira yake yameharibiwa vibaya kwa kuchomwa moto hali ambayo imesababisha viumbe kama Nyuki wamekimbia msituni na kukaa katika makazi ya watu ili kujinusuru.

Mkuu wa wilaya ya Ludewa Bw.Juma Solomon Mdaha hivi karibuni aliweza kuwaita maafisa watendaji wa vijiji na kuwataka kuwakamata mara moja watu wanaohusika na uchomaji moto huo holela.

Bw.Madaha anasema sababu kubwa ya misitu ya wilayani kwake kuharibiwa ni kutokana na msimu wa kilimo kukaribia hivyo wakulima wanaoandaa mashamba yao kwaajili ya kulima mazao ya mahindi na ngano wamekuwa wakiyandaa mashamba hayo kwa kuyachoma moto.

Anasema pindi wakulima waandaapo mashamba hayo moto huwatoroka na kuchoma misitu hali inayosababisha kutokana na sheria kuwabana baadhi yao hutoroka na kuziacha familia zao katika hali ya upweke kwa kuhofia kufungwa magerezani.

Alizitaja sababu nyingine ni uwindaji wa wanyama poli na uchomaji mkaa,kuna wananchi wengine ni wawindaji hivyo kutokana na kuwepo kwa nyasi ndefu maeneo wanayowindia hulazimika kuzichoma nyasi hizo ili kupata urahisi wa kuwawinda wanyama hao.

Kuhusiana na suala la uchomaji mkaa mkuu wa wilaya Bw.Juma Solomon Madaha anasema tatizo hilo lipo kwani wachomaji wa mkaa hupalua mkaa unaokuwa na moto na kusambaza ili moto huo uzime hali inayosababisha moto huo kuangukia katika nyasi na kusambaa misituni.

“baadhi ya wananchi bado hawana elimu ya kutosha kuhusu uhifadhi wa mazingira hivyo nimewaagiza watendaji wa kata na vijiji kutoa elimu hiyo na kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wenye tabia ya kuharibu mazingira kwa kuchoma moto hovyo misitu isiyo na hatia”,alisema Bw.Madaha.

Anasema hakuna njia rahisi ya kufikisha elimi ya uhifadhi wa mazingira kwa wananchi walio vijijini zaidi ya vyombo vya habari na watendaji wa Serikali ambao huishi na wananchi huko vijijini kwa kufanya hivyo hakuna litakalo shindikana kwani halihalisi ya athari za uharibifu wa mazingira zimeshaanza kuonekana.

Alizitaja athari hizo ambazo zimeshaanza kuonekana wilaya Ludewa ni pamoja na kukosekana kwa maji safi na Salama kutokana na miundombinu ya maji iliyoko katika vyanzo vya maji ambavyo vipo misituni kuharibiwa kwa moto.

Bw.Madaha alisema wananchi wamekuwa waitupia lawama Serikali kutokana na ukosefu wa huduma ya maji safi na salama kitu ambacho si kweli suala kubwa lilalosababisha hali hiyo itokee wilayani Ludewa ni uharibifu wa mazingira hasa uchomaji moto miundombinu ya maji.

Alisema Serikali wilayani Ludewa inaingia gharama za ununuzi wa bomba za maji pasipo sababu za msingi kwani wananchi wakielimishwa lawama Serikalini zitapungua kutokana na tatizo la ukosefu wa maji linavyozidi kukua siku zinavyoendelea.

Iko haja ya kufanya kampeni kwa kutumia vikundi vya sanaa huko vijijini ili kuelimisha wananchi umuhimu wa kuyatunza mazingira yao kwa kutochoma moto hovyo na kuacha tabia ya kulima katika vyanzo vya maji.

Alisisitiza hivi karibuni wananchi wameshindwa kupata maji safi na salama kwa muda wa wiki mbili sababu kubwa ikiwa ni kuungua kwa miundimbinu ya maji kutoka katika vyanzo vya maji yanayosambazwa katika mji wa Ludewa.

Hivyo wananchi ndio wa kulaumiwa na si Serikali kama wengi wengi wanavyofikiri,kwani upande wa Serikali wanatekeleza wajibu wao lakini wananchi ndio chanzo kikubwa katika uharibifu wa mazingira kwa kuchoma moto hovyo hali inayosababisha kuwepo hali ya ukame katika maeneo mazuri ya kilimo.

Chesko Mlelwa mwnanchi wa kijiji cha Amani wilayani Ludewa akiwa yeye ni mfugaji alisema hali kwa sasa imekuwa mbaya zaidi kwa upande wa malisho ya Mifugo kwani maeneo ya kuchungia yameteketezwa kwa moto na wakulima.

Bw.Mlelwa alisema imefika wakati wanalazimika kuhama na kwenda katika maeneo ya mito ambako ndiko kuna vyanzo vya maji kwa wananchi nao hutegemea huko katika kupata maji kwaajili ya matumizi ya nyumbani.

“Wananchi wamekuwa wakitumia maji pamoja na mifugo yao katika matumizi ya kila siku hali ambayo inaweza kusababisha binadamu tukaugua magonjwa ya ajabu kwani awali kulitengwa  maeneo ya mifugo na wanadamu kwa sasa hakuna tena”,alisema Bw.Mlelwa.

Alisema hali hii itazidi kuwa mbaya zaidi kama mvua zitachelewa kunyesha kwani mazingira yameharibiwa vibaya na uchomaji moto hovyo unaoashilia kuwepo na jangwa kwa miaka ya baadae wilayani Ludewa.

Mama Lusiana Haule wa kijiji cha Nkomang’ombe wilayani Ludewa ni mmoja kati ya akina mama wanaopata shida ya upatikanaji wa maji safi na salama unaosababishwa na uharibifu wa mazingira wilayani humo.

Mama Lusiana alisema hali ya mwaka huu 2013 imekuwa mbaya zaidi kwani hulazimika kuamka saa nane usiku kwena kisimani kusubiri maji kutokana na mito kukauka kwa sababu ya uharibifu wa mazingira uliokithiri.

Alisema safari ya kuyatafuta maji huanza kuanzia saa nane usiku kwa akina mama wa kijiji hicho ambapo hukaa kisimani na kurudi saa kumi na moja Alufajiri kwani bila kufanya hivyo unaweza usifanye chochote kuwa siku hiyo.

“Tumekuwa tukikesha visimani na watoto wetu ili kuhakikisha tunapata maji safi na salama kwani bila kufanya hivyo familia hushinda bila kula lakin I sababu kubwa ya yote hayo ni uharibifu wa mazingira unaoendelea siku hadi siku tofauti na zamani kulikuwa na maji maengi kila pahala”,alisema mama Lusiana.

Kutokana na hali hiyo ya kutumia muda mwingi kutafuta maji kuna baadhi ya wanafunzi wa shule za msingi huungana na wazazi wao kukesha visimani na kushindwa kuhudhuria masomo kwani kila siku hurudi nyumbani asubuhi.




No comments: